1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

EURO 2024: Mbappe ahofia wapinzani kuilenga pua yake

1 Julai 2024

Nahodha wa Ufaransa Kylian Mbappe hatoshangaa iwapo pua yake iliyovunjika italengwa na wapinzani katika mechi yao Jumatatu watakapocheza na Ubelgiji.

https://p.dw.com/p/4hkAP
Euro 2024 Fussball EM l Österreich vs Frankreich l Kylian Mbapp verletzt
Kylian Mbappe baada ya kupata jeraha la puaPicha: Alessandra Tarantino/AP/picture alliance

Mechi hiyo itakuwa ni ya hatua ya mtoano ya kumi na sita bora ya mashindano ya Ulaya ya Euro 2024.

Mbappe lakini anasema anadhamiria kucheza na jeraha hilo na maumivu aliyo nayo na kuhakikisha kwamba timu yake inapata ushindi kwenye mechi hiyo itakayochezwa huko Düsseldorf.

Akizungumza na waandishi wa habari tangu apate jeraha hilo katika mechi dhidi ya Austria, Mbappe amesema kwamba awali alikuwa na hofu kwamba huenda akakosa kushiriki kabisa mashindano haya ya Ulaya.

Deutschland Leipzig | Euro 2024 BG | Kylian Mbappe mit Maske
Mbappe kwa sasa anatumia barakoaPicha: Koen van Weel/ANP/picture alliance

"Nafikiri unapocheza na pua iliyovunjika baada ya kuamua usifanyiwe upasuaji, unakuwa mlengwa ingawa sidhani kama Lewandowski alikusudia kunigonga. Ila kwa kweli nilijua nitakachopambana nacho nilipoamua niendelee kucheza badala ya kufanyiwa upasuaji," alisema Mbappe.

Licha ya kikosi kipana na wachezaji mahiri walio nao na juu yake kuingia kwenye mashindano haya wakiwa timu iliyokuwa inapigiwa upatu na wengi kuibuka mabingwa, Ufaransa haijafunga magoli mengi kufikia sasa.

Na sasa kocha wa Le Bleus Didier Deschamps anasema wachezaji wake wanastahili kuhakikisha kwamba wanazitumia vyema nafasi watakazozibuni katika mechi ya leo dhidi ya Ubelgiji.

"Kushinda mechi, unastahili kufunga na hatujaweza kufanya hivyo. Ila jambo hili linaweza kufanyika katika timu, linafanyika hata kwa wafungaji wote mahiri. Sijizungumzii mimi ila unaweza kwenda mechi nne, tano au hata sita bila kufunga," alisema Deschamps.

Vyanzo: Reuters/DPAE