1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mashambulizi ya anga yautikisa mji mkuu wa Sudan, Khartoum

25 Juni 2023

Milio ya risasi na mashambulizi ya anga yameutikisa mji mkuu wa Sudan, Khartoum huku Umoja wa Mataifa ukihimiza kusitishwa kwa "mauaji ya kiholela" ambayo yameacha miili ya watu ikitapakaa katika jimbo la Darfur.

https://p.dw.com/p/4T20I
Sudan | Konflikt im Sudan
Picha: picture alliance/dpa/AP

Wakizungumza na shirika la habari la AFP baadhi ya wakaazi wamesema wilaya zote za Khartoum hazina tena maji ya bomba, na wale waliosalia katika jiji hilo hawana umeme kabisa tangu Alhamisi.

Kulingana na shirika linalojishughlisha na ukusanyaji na uchambuzi wa taarifa katika maeneo ya mizozo la ACLED,  Vita vya kugombea madaraka kati ya mkuu wa jeshi Abdel Fattah al-Burhan na makamu wake wa zamani, kamanda wa RSF Mohamed Hamdan Daglo, vimesababisha vifo vya zaidi ya watu 2,000.

Kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa takriban watu milioni 1.5 wameukimbia mji mkuu Khartoum tangu kuzuka kwa ghasia nchini humo katikati ya mwezi wa Aprili.

Hadi sasa, hakuna upande unaoonekana kuwa tayari kusitisha mapigano na hivyo kuzidisha hatari ya mzozo wa muda mrefu wa kikanda.