1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais wa Iran ateua gavana wa kwanza Msunni katika miaka 45

18 Septemba 2024

Rais mpya wa Iran Masoud Pezeshkian, Jumatano alimteua Muislamu wa madhehebu ya Sunni, Arash Zerehtan kuwa gavana wa mkoa wa Kurdistan.

https://p.dw.com/p/4klc8
Kurdistan ya Iran 2024 | Arash Zerehtan Lahouni gavana mpya
Arash Zerehtan anakuwa gavana wa kwanza Muislamu wa madhehebu ya Sunni nachini Iran katika miaka 45.Picha: Hammihan

Arash Zerehtan aliteuliwa kuwa mkuu wa mkoa wa magharibi, shirika la habari la IRNA lilisema, likimnukuu msemaji wa serikali Fatemeh Mohajerani.

Yeye ndiye Msunni wa kwanza kufanywa gavana wa eneo katika nchi hiyo yenye Washia wengi tangu siku za mwanzo kabisa za Mapinduzi ya Kiislamu ya 1979.

Zerehtan, mwenye umri wa miaka 48, aliwahi kuwa mbunge wa jiji la Paveh kati ya 2020 na mwaka huu.

Wasunni wanachangiaa takriban asilimia 10 ya wakazi wa Iran, ambao wengi wao ni Mashia na Uislamu wa Shia ndio dini rasmi ya taifa.

Iran Teheran | Rais Masoud Pezeshkian
Rais wa Iran amekuwa akinyoosha mkono kwa makundi ya wachache na kuyajumuisha katika uongozi wake.Picha: Vahid Salemi/dpa/AP/picture alliance

Ni mara chache sana wameshika nyadhifa muhimu za madaraka tangu mapinduzi.

Soma pia: Masoud Pezeshkian aidhinishwa kuwa Rais wa Iran

Pezeshkian, mwenye umri wa miaka 69, aliingia madarakani Julai baada ya uchaguzi wa mapema kufuatia kifo cha rais wa kihafidhina Ebrahim Raisi katika ajali ya helikopta.

Wakati wa kampeni zake za uchaguzi, Pezeshkian alikosoa ukosefu wa uwakilishi kwa jamii za wachache wa kikabila na kidini, hasa Wakurdi wa Kisunni, katika nyadhifa muhimu.

Mnamo Agosti, alimfanya mwanachama mwingine wa Madhehebu ya Wasunni walio wachache, Abdolkarim Hosseinzadeh, kuwa mmoja wa makamu wake wa rais.