1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Je, EU inapaswa kufikiria upya sera yake kuhusu Syria?

22 Agosti 2024

Ikiwa ni takribani muongo mmoja tangu kuzuka kwa mzozo wa Syria na miaka kadhaa baada ya mzozo wa kijeshi kutulia, Wasyria wanaendelea kuwa moja ya makundi makubwa ya wahamiaji wanaotafuta hifadhi kwa nchi Ulaya.

https://p.dw.com/p/4jnGw
Umoja wa Ulaya | Josep Borrell
Mkuu wa Sera za Kigeni wa Umoja wa Ulaya Josep BorrellPicha: Zheng Huansong/Xinua/IMAGO

Sera ya Umoja wa Ulaya kuhusu Syria imeshindikana na Rais Bashar al-Assad ameshinda. Hilo halimaanishi kuwa nchi wanachama wa umoja huo zitaifuata Italia na kupeleka mjumbe wao Damascus, lakini zimechelewa kufikiria upya kuhusu sera hiyo.

Kulingana na Shirika la Kutafuta Hifadhi la Umoja wa Ulaya, zaidi ya maombi milioni moja ya waomba hifadhi yaliwasilishwa mwaka uliopita katika nchi ambazo sio wanachama wa Umoja wa Ulaya, lakini zina ushirikiano na umoja huo, zikiwemo Norway na Uswisi, idadi ambayo ni ongezeko la asilimia 18 ikilinganishwa na mwaka 2022.

Shirika hilo limesema idadi hiyo inakumbushia mzozo wa wakimbizi wa mwaka 2015 hadi 2016, na maombi mengi yamewasilishwa na Wasyria, hadi asilimia 38 ikilinganishwa na mwaka uliotangulia.

Wataalamu kadhaa wameiambia DW kuwa, huku sera hiyo ilitegemewa kuleta matumaini ya kuleta mabadiliko kwa serikali ya Bashar al-Assad na kuihimiza kuzingatia demokrasia na kuimarisha rekodi ya haki za binaadamu, imeshindwa kuyafikia yote hayo.

Soma pia:Shambulio la Israel Damascus lauwa makamanda wa Iran

Badala yake vikwazo vinaweza kuwa vimepunguza zaidi ya matarajio ya kiuchumi ya nchi hiyo ambayo tayari imeharibiwa kwa vita na kuongeza sababu zinazochochea uhamiaji.

Wataalamu wanasema kufikiria upya sera ya Umoja wa Ulaya kuhusu Syria kumechelewa, lakini wanakiri kuwa nchi wanachama ziko katika wakati mgumu.

Jinsi ya kupunguza idadi ya namba za wahamiaji, na wakati huo huo kujiepusha kuzungumza na Assad anayetuhumiwa kwa uhalifu wa kivita dhidi ya watu wake.

Mtaalamu: EU inapaswa kurekebisha uhusiano wake na Assad

Wengine wanasema kuongezeka kwa siasa kali za mrengo wa kulia na uhamiaji, kunaendelea kuwa suala kuu la kisiasa barani Ulaya, na suala la kuimarisha uhusiano na Assad linakuja baadae.

Joshua Landis, Profesa na Mkurugenzi wa Kituo cha Mafunzo ya Mashariki ya Kati katika Chuo Kikuu cha Oklahoma, amesema kuwa Ulaya hatimaye itabidi kufuata na kurekebisha uhusiano na Assad, na suala hilo halitokuwa hivi karibuni, lakini litakuja.

Wabunge wa Bunge la Ulaya wakiwa bungeni.
Wabunge wa Bunge la Ulaya wakiwa bungeni.Picha: Johannes Simon/Getty Images

Mwezi uliopita, nchi nane za Ulaya zilimtaka Mkuu wa sera za kigeni za Umoja wa Ulaya, Josep Borel kumteua mjumbe wa umoja huo kwa ajili ya Syria, na kutenga maeneo kumi salama ya kuwarejesha Wasyria.

Mawaziri wa mambo ya nje wa Austria, Croatia, Jamhuri ya Czech, Cyprus, Ugiriki, Slovenia na Slovakia, walisaini kwa pamoja barua hiyo, huku Italia ikienda mbali zaidi na kutangaza kuwa itapeleka mjumbe wake Damascus.

Soma pia:Mjumbe wa UN nchini Syria awasihi wafadhili wasisitishe misaada

Waziri wa Mambo ya Nje wa Italia, Antonio Tajani amesema wazo la kurejesha uhusiano na Syria, pengine kwa vile Umoja wa Ulaya umekuwa ukijihusisha na migogoro ya Ukraine na Gaza katika miaka michache iliyopita. Stefano Ravagnan, ambaye kwa sasa ni mjumbe maalum wa wizara ya mambo ya nje nchini Syria, ameteuliwa kuwa balozi.

Kulingana na vyanzo vya habari, Ujerumani na Ufaransa zilizuia njia hiyo, lakini kuongezeka kwa siasa kali za mrengo wa kulia kwenye maeneo kadhaa ya nchi za Umoja wa Ulaya, kama ilivyodhihirika katika uchaguzi wa bunge la Ulaya hivi karibuni, na Italia kwenyewe ambako ina chama cha mrengo wa kulia kinachoongoza, kunaonekana kuipa italia nafasi ya kushinikiza uamuzi huo wenye utata.

Aron Lund kutoka Wakfu wa Century, ameiambia DW kuwa hata serikali za Ulaya ambazo zingependelea kumsusia Assad kabisa, sasa zinahitaji kuzingatia maana ya uhamiaji.

EU katika kudhibiti wimbi la wahamiaji

Mapema mwaka huu, bunge la Umoja wa Ulaya lilipitisha mkataba mpya wa waomba hifadhi na uhamiaji ili kudhibiti vizuri na kuratibu usimamizi wa waomba hifadhi. Umoja huo ulikubali kulipa kiasi kikubwa cha fedha kwa Tunisia na Misri ili kupunguza kuingia kwa wahamiaji.

Denmark ilikuwa nchi ya kwanza kuamua kuwarejesha nyumbani baadhi ya Wasyria, baada ya kutangaza sera ya kupunguza idadi ya waomba hifadhi.

Rais Assad uso kwa uso na viongozi mataifa ya Kiarabu

Mtaalamu wa masuala ya uhamiaji kutoka Sweden, Bernd Parusel ameiambia DW kuwa Sweden pia ilianzisha sera kali zilizokusudiwa kuwakatisha tamaa wanaotafuta hifadhi kutuma maombi yao.

Soma pia:UN yasema imeafikiana na Syria kuhusu uingizaji misaada

Mwezi Juni, Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz alionyesha kuwa serikali yake ilikuwa inatafuta njia za kuwafukuza wahalifu waliokutwa na hatia, hata wale wanaotokea Syria.

Hata hivyo, ripoti iliyotolewa mwezi Februari na Ofisi ya Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa ilionesha taswira ya kutisha sana ya hali inayowakabili watu wanaorejea Syria.

Ripoti hiyo ilieleza kuwa Wasyria wengi wanaorejea nyumbani, walikimbilia tena nchi kama vile Uturuki au Lebanon, na kwamba hali jumla nchini Syria bado hairuhusu watu kurudi kwa sababu sio salama.