1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Senegal yasimamisha uchimbaji madini katika mpaka na Mali

28 Agosti 2024

Senegal imesimamisha kwa muda shughuli za uchimbaji madini kwenye ukingo wa mto ambao ni sehemu ya mpaka wake wa kusini mashariki na Mali.

https://p.dw.com/p/4k0DX
Rais wa Senegal Bassirou Diomaye Faye
Rais wa Senegal Bassirou Diomaye FayePicha: Luc Gnago/REUTERS

Senegal imesimamisha kwa muda shughuli za uchimbaji madini kwenye ukingo wa mto ambao ni sehemu ya mpaka wake wa kusini mashariki na Mali. Hatua hizo zinalenga kuhifadhi mazingira na kulinda afya za wenyeji. Mto Faleme, kijito kikuu cha Mto Senegal, unakabiliwa na uchafuzi mkubwa wa mazingira kutokana na matumizi makubwa ya kemikali katika migodi ya dhahabu ambayo inashamiri katika eneo hilo. Maelfu ya watu wanautegemea mto huo kwa shughuli za kilimo na kulisha mifugo.

Soma: Senegal yaanza uzalishaji wake wa kwanza wa mafuta

Marufuku hiyo ya miaka mitatu, ambayo itadumu hadi Juni 30, mwaka 2027, itajumuisha eneo la mita 500 kando ya ukingo wa kushoto wa mto Faleme. Mchakato wa utoaji wa vibali vya uchimbaji madini pia umesitishwa. Eneo la kusini mashariki mwa Senegal la Kedougou, limekuwa likikumbwa na wimbi la watu wanaowasili kwa ajili ya kuchimba dhahabu kwa takriban miaka 20, huku maelfu wakitoka kote Afrika Magharibi.