1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroMali

Watu zaidi ya 70 waliuawa shambulio la Bamako

Sylvia Mwehozi
19 Septemba 2024

Duru za kiusalama nchini Mali zimesema kwamba zaidi ya watu 70 waliuawa katika shambulio la wiki hii lililofanywa na wapiganaji wenye itikadi kali katika mji mkuu wa Bamako na kuwajeruhi watu wengine zaidi ya 200.

https://p.dw.com/p/4krRH
Silaha zilizokamatwa katika shambulio la mjini Bamako
Silaha zilizokamatwa katika shambulio la mjini BamakoPicha: ORTM/AFP

Kulingana na chanzo kimoja cha usalama kilichozungumza na shirika la habari la AFP kwa sharti la kutotambulishwa, kimesema watu 77 waliuawa na 255 walijeruhiwakatika shambulio la Jumanne mjini Bamako. Gazeti moja la kila siku nchini humo Le Soir limeripoti leo kwamba kunafanyika mazishi ya wanafunzi takribani 50 wa chuo cha kijeshi.

Hadi kufikia sasa mamlaka za serikali ya Mali inayoongozwa kijeshi hazijatoa takwimu rasmi za watu waliouawa katika shambulio hilo linalodaiwa kufanywa na kundi lenye mafungamano na Al-Qaeda la Jama'at Nusrat al-Islam wal Muslimeen JNIM. Lakini mamlaka hizo zilikiri kwamba wapo watu waliopoteza maisha haswa wafanyakazi katika kituo cha mafunzo ya kijeshi.

Jeshi la Mali ladhibiti usalama baada ya shambulio Bamako

Kundi la JNIM pia lilidai wapiganaji wake kadhaa waliuawa na kuwaua "mamia" kutoka upande wa serikali wakiwemo wanachama wa kundi la wapiganaji mamluki wa Urusi Wagner. 

Shambulio hilo lilitokea siku moja baada ya nchi zinazoongozwa kijeshi za Mali, Niger na Burkina Faso kuadhimisha mwaka mmoja tangu zilipoanzisha muungano wao mpya wa mataifa ya Sahel AES. Baadhi ya wakaazi wa Bamako bado wana mashaka na suala la usalama, kama anavyoeleza mchuuzi huyu Sidi Maiga.  "Hakuna uhakika wa usalama. Jinsi kambi ilivyoshambuliwa, kama tusingekuwa na askari wenye uzoefu, magaidi wangekidhibiti kituo. Na vipi kuhusu sisi raia?" SomaMashambulizi ya wanajihadi Mali yazusha ukosoaji, maswali

Hayo yakiarifiwa, Shirika la Mpango wa Chakula WFP limesema ndege iliyokuwa ikitumiwa kwa ajili ya shughuli za kiutu iliharibiwa wakati wa shambulio hilo. Ndege hiyo inamilikiwa na kampuni ya Afrika Kusini ya National Airways ambayo "ilishambuliwa" wakati ilipokuwa imetua mjini Bamako. Taarifa ya kampuni hiyo imeongeza kwamba timu na wafanyakazi hawajadhurika na wako salama. Kwa mujibu wa shirika la WFP ndege hiyo ilikuwa ikitumiwa "kusafirisha wafanyakazi wa kiutu na kutoa misaada ya dharura ya kibinadamu katika maeneo ya ndani ndani huko Mali".

Mali Bamako
Maafisa wa usalama wa Mali wakimshikilia mtu baada ya jeshi la Mali kusema kuwa kambi ya mafunzo ya kijeshi katika mji mkuu Bamako imeshambuliwaPicha: AP Photo/picture alliance

Katika hatua nyingine mwenyekiti wa Halmashauri ya Umoja wa Afrika Moussa Faki Mahamat "amelaani vikali" mashambulizi hayo ya wapiganaji wenye itikadi kali dhidi ya Mali.Jeshi la Mali ladhbiti hali Bamako kufuatia shambulizi

Katika taarifa yake, Mahamat ametoa "wito wa dharura wa kuimarisha ushirikiano wa kimkakati wa kikanda na kimataifa katika mapambano dhidi ya kuzuka upya kwa ugaidi" katika kanda ya Afrika Magharibi. Jumuiya ya kiuchumi ya Mataifa ya Afrika Magharibi ECOWASnayo ililaani vikali mashambulizi hayo na kusisitiza "dhamira yake kubwa ya kuunga mkono mpango wowote" wa kuleta amani.

Vyanzo: AFP/AP