1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Saudi Arabia yaunda mabaraza mapya Yemen Kusini

Jennifer Holleis Saumu Mwasimba
6 Julai 2023

Wafuasi wa kisiasa wanaopingana wanataka kuongeza ushawishi wao katika mji muhimu kimkakati wa Aden. Waangalizi wanaona nyuma ya hili, kuanza kwa mkakati wa Saudi Arabia kujitoa katika vita nchini Yemen.

https://p.dw.com/p/4TWSn
Lokale (Stammes-)Mediationen im Jemen
Picha: DW

Kwa mujibu wa shirika la habari la Yemen, baraza la kwanza la utawala linaloungwa mkono na Saudi Arabia limeshaanzishwa  katika eneo la Hadramaut mnamo mwezi Juni.

Na baraza jingine kama hilo limepangwa kuanzishwa Julai katika mji wa bandari wa Aden. Pindi taasisi hizo mbili zinazoungwa mkono na Saudi Arabia zitakamilika basi zitakuwa tayari kuitia nguvu fikra ya kuiunganisha Yemen.

Yemen imekuwa vitani tangu mwaka 2014 baada ya waasi Wakihouthi wanaoungwa mkono na Iran kuudhibiti mji mkuu Sanaa na kuiangusha madarakani serikali iliyokuwepo nchini.

Mnamo mwaka 2015 hali ikatibuka zaidi baada ya muungano wa kijeshi uliojumuisha nchi tisa, ukiongozwa na Saudi Arabia kuingilia kati nchini Yemen kutaka kuirudisha madarakani serikali iliyotambuliwa Kimataifa.

VAE | Kronprinz Scheich Mohammed bin Sajed
Rais wa UAE Mohammed bin Zayed al-Nahyan. Taifa lake linaunga mkono baraza linalopigania kujitenga kwa Yemen Kusini.Picha: Thomas Samson/AFP/Getty Images

Umoja wa falme za kiarabu ni miongoni pia mwa nchi zilizounda muungano huo wa kijeshi wa kupambana na Wahouthi wakiungwa mkono na Iran.

Umoja huo wa falme za kiarabu ni mshirika thabiti wa Saudi Arabia isipokuwa wanatofautiana linapokuja suala la wanaotaka kujitenga Kusini mwa Yemen.

Baraza la mpito kusini mwa Yemen ambalo linapigania kujitenga na Yemen linaungwa mkono na Umoja wa Falme za Kiarabu

Yemen imegawanywa mapande matatu kufikia sasa, upande wa kwanza ukiwa ule wa Kaskazini, unaodhibiti na waasi wa Kihouthi.

Soma piaMkanyagano Yemen wakati wa kutolewa msaada wauwa watu 85

Upande wa Kusini uko chini ya baraza la mpito linaloungwa mkono na Umoja wa Falme za Kiarabu wakati sehemu nyingine yote ya nchi iliyobakia inashikiliwa na serikali inayoungwa mkono na muungano wa kijeshi unaoongozwa na Saudi Arabia.

Mashaka juu ya ufanisi wa mabaraza ya Saudi Arabia

Hivi sasa Saudi Arabia imeanzisha mabaraza mawili ya utawala kwa lengo la kuiunganisha Yemen, lakini baadhi ya wataalamu wa siasa za kanda hiyo wanatilia mashaka hatua hiyo na ikiwa itafanikiwa.

Matthew Hedges, mtafiti kuhusu Yemen na kanda hiyo ya Ghuba kwa ujumla anayeishi London, Uingereza ameiambia DW, kwamba muda wa kuanzishwa juhudi hizi ni muhimu.

Anasema  katika wakati huu ambapo juhudi za mazungumzo ya amani kati ya Saudi Arabia na waasi Wakihouthi wanaoungwa mkono na Iran zikionekana kushindwa na Saudi Arabia ikitaka kujiingiza upande wa Kusini mwa Yemen, inaweza kuwa ishara ya Saudi Arabia kukiri kwamba Yemen huenda ikagawika mapande mawili.

Saudi-Arabien | Jemens Präsident Abd-Rabbu Mansour Hadi hält eine Rede
Raisw a Yemen Abd-Rabbu Mansour Hadi anaeungwa mkono na Saudi Arabia na UAE.Picha: Yemen TV/REUTERS

Wanaofuatilia hali ya mambo, hata hivyo kwahakika wanatilia shaka kwamba haya mabazara mapya yatakuwa na athari katika misimamo ya kisiasa upande wa Kusini.

Soma pia: Mamia ya wafungwa waachiwa huru Yemen

Hedges ameiambia Dw kwamba haoni uwezekano kwa baraza jipya la Aden kushamiri na kuwa na uungaji mkono wa jamii au kutanuka na kuwa vuguvugu la kisiasa ambalo linaweza kulikabili baraza la mpito la uongozi wa Kusini.

Na kwahakika kwa mtazamo wake anayaona haya mabaraza mapya ni sawa sawa na kile alichokiita kumuweka paka katikati ya kundi la njiwa.''

Mtazamo wa Hedges unaungwa mkono na Mohammed al Iriniani, mchambuzi wa masuala ya utafiti katika kituo cha sera nchini Yemen, ambayo ni taasisi huru ya utafiti mjini Sanaa.

Anasema Saudi Arabia imefanya mara kadhaa juhudi za kuunda mungano wa kisiasa kwenye eneo la Aden na hasa muungano unaojumuisha makundi ya kisiasa ambayo yana azma inayofanana ya kuiunganisha Yemen kuwa kitu kimoja, lakini Juhudi hizo hazikuwahi kufanikiwa.

Soma pia: Wasaudia wakutana na waasi wa Houthi kutafuta amani Yemen

Hata hivyo mtafiti huyo kuna kitu kimoja anachokiona kinaweza kuletwa na mabaraza hayo mapya yanayoungwa mkono na Saudi Arabia.

Karte Jemen Saudi Arabien EN
Ramani inayoonyesha mipaka ya Yemen.

Tofauti za Saudi na UAE Yemen

Kwa mtazamo wake ikiwa Saudi Arabia na Umoja wa Falme za Kiarabu watafanikiwa kuondowa tafauti zao upande wa Kusini basi mabaraza hayo mapya  huenda yakawa na uwezekano wa kuleta maridhiano katika midahalo ya ndani baina ya makundi ya Kusini.

Na juu ya hilo mtaalamu huyo anaamini ni hatua inayoweza kuusadia muungano wa kijeshi unaoongozwa na  Saudi Arabia kujiondowa kwenye vita vya Yemen.

Vita hivyo vya umwagaji mkubwa wa damu,ambavyo kimsingi vinaendelea licha ya kuwepo utulivu kiasi kwa kiasi kikubwa vimeonekana kuwa ni vita baina ya mataifa mawili hasimu,Saudi Arabia na Iran.

Japokuwa Saudi Arabia imezidi kujionesha wazi kwamba inatamani kujiondowa kwenye vita hivyo vya gharama kubwa.

Na uwezekano huo umepata nguvu zaidi baada ya Riyadh na Tehran ambazo zilikuwa wakati mmoja maadui wakubwa, wasiotazama kwa macho, kurejesha mahusiano ya kidiplomasia March mwaka huu.

Chanzo: DW